Search This Blog

TANZANITE CITY: The Africa's Factory & Innovation Powerhouse!

TANZANITE CITY: The Africa's Factory & Innovation Powerhouse!
We Will Turn Bushes Into Highly Industrialized City

Sunday, October 8, 2017

Salaam za pongezi kwa Mh. Dr. Mary Mwanjelwa (Naibu Waziri Mteule wa Kilimo)


Mheshimiwa Dr. Mary Mwanjelwa, Naibu Waziri Mteule Wa Kilimo

Kamati ya uongozi inayoshugulikia ujenzi wa jiji la sayansi, teknolojia na ubunifu la Tanzanite City – Chunya, pamoja na wadau wetu wote kupitia klabu ya marafiki wa Tanzanite City, tunapenda kutoa pongezi zetu za dhati kabisa kwa mbunge wetu wa Mbeya na mdau wa Tanzanite City, Mheshimiwa Dr. MARY MWANJELWA kwa kuteuliwa kwake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Pombe Magufuli Kuwa Naibu Waziri wa Kilimo.
Tunatambua uwezo mkubwa sana alionao Mh. Mwanjelwa katika kutekeleza majukumu yake. Sisi kama wadau wa maendeleo ya viwanda na Teknolojia tunatambua jukumu kubwa na zito analokwenda kulibeba Mh Mwanjelwa, si mchezo-mchezo bali anatakiwa kuwa mbunifu sana na asiyechoka kujifunza. Nchi yetu ni kubwa sana na ina matatizo mengi mno yanayohusiana na wizara anayokwenda kuifanyia kazi.
Moja ya changamoto ambazo Mh. Naibu Waziri atakutana nazo katika utekelezaji wa majukumu yake ni matumizi duni ya teknolojia katika kilimo kwa ujumla wake na namna ya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo. Katika wakati huu ambao taifa letu lipo kwenye kipindi cha mpito kuelekea uchumi wa kiviwanda, suala la teknolojia linapaswa kupewa kipaumbele kwani linagusa kila Nyanja ya kilimo, kuanzia kwenye maandalizi ya ardhi ikiwa ni pamoja na kuilima, kupanda na kupandikiza mazao mashambani, kutunza mazao yaliyoshambani ili yaweze kutoa matunda bora na ya kutosha, uvunaji wa mazao na kuyasafirisha toka mashambani, uhifadhi wa mazao ghafi ya kilimo pamoja na kuyaongezea thamani. Yote hayo yanahitaji teknolojia kwa mapana yake!
Mh. Naibu Waziri, ni vigumu sana kuweza kuendelea kama taifa, iwe ni kwenye kilimo, viwanda au hata biashara tu, iwapo tutapuuza matumizi ya teknolojia. Lakini pamoja na kutilia maanani matumizi hayo ya teknolojia, bado hatutaweza kufikia malengo yetu ya kiuchumi kama tutaendelea kuwa tegemezi kwa kiteknolojia toka nje. Kwani hao tunaowategemea wao pia wanavyo viapaumbele vyao ambavyo siyo lazima vifanane na vyetu. Hivyo sasa ni jukumu letu kama kweli tunataka kwenda kwenye uchumi wa kati, wa viwanda na kilimo cha kibiashara na chenye tija, kuanza sasa kujenga uwezo wetu wenyewe kwenye mambo ya technolojia ambao ndiyo mhimili wa hivyo viwanda na hicho kilimo tunachokitaka.
Mh. Naibu Waziri, sisi tumeanza na Tanzanite City, ni safari ngumu na ndefu, lakini tumedhamiria kufika mwisho, tunaamini kuwa, kwa kuwekeza kwenye vipaji vya vijana wetu, na kuwasaidia kutimiza ndoto zao, tutabadilisha mustakabari wa taifa letu na kuboresha sana kilimo chetu, tukishirikiana sisi wanachi, wadau wa maendeleo, pamoja na serikali tunaweza kuifanya Tanzania kuwa kiwanda cha Afrika, na kitovu cha ubunifu katika maswala ya teknolojia.
Mh. Naibu Waziri, tuna jua NIA UNAYO, SABABU UNAYO NA UWEZO UNAO! Tunakuahidi ushirikiano wetu, tunakuombea afya njema, hekima, na heshima kwa watu unaowaongoza, wengi wamepita na hawajaacha alama yoyote baada ya wao kuondoka, na wewe hutaishi milele kwenye hiyo nafasi, lakini tunatamani kuona alama za kazi zako zikidumu daima kwa vizazi vingi vijavyo!! TUNAJUA NA TUNAAMINI UNAWEZA!!! Tuna kutakia kila lililo la heri, ufanikiwa katika majukumu yako hayo kwa taifa letu, MUNGU Akubariki na akulinde siku zote za maisha yako. Amina.