Search This Blog

TANZANITE CITY: The Africa's Factory & Innovation Powerhouse!

TANZANITE CITY: The Africa's Factory & Innovation Powerhouse!
We Will Turn Bushes Into Highly Industrialized City

Monday, November 25, 2013

Kama tunapenda maendeleo, tuwekeze katika utafiti wa viwanda mama!

Tunapozungumzia teknolojia tuangalie katika namna kubwa mbili; Teknolojia ya viwanda vinavyozalisha bidhaa za mwisho kwa ajili ya walaji, Teknolojia ya viwanda mama vinavyozalisha mitambo na mashne za uzalishaji
Taifa letu hivi sasa lina umri wa miaka 50 tangu tupate uhuru toka kwa mkoloni, mpaka sasa hakuna uwekezaji wowote wa uhakika uliofanywa katika kukuza teknolojia ya viwanda nchini zaidi ya ule uliofanyika wakati wa awamu ya kwanza ya uongozi wa taifa letu iliiyoongozwa na hayati baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Uwekezaji katika namna ya Kwanza ya teknolojia ni rahisi kidogo kwani hutegemea zaidi na hali na mazingira ya soko, aina ya bidhaa na uwezo wa mtaji wa mwekezaji. Uwekezaji huu unaweza kufanywa na mtu yoyote, ni wa kibiashara zaidi na unalenga kuzalisha bidhaa mahususi. Taifa linapojikita zaidi katika uwekezaji wa namna hii litakabiliwa na matatizo yafuatayo; Mitambo na mashine za viwanda hivi hununuliwa kama zilivyo toka nchi zinakotengenezwa, taifa linalonunua linategemezi kiteknolojia kwa vile muuzaji wa mitambo hiyo ndiyo mwenye teknolojia na ndiyo wanaofanya tafiti na kuendeleza teknolojia hiizo, Taifa linapowekeza katika viwanda vya namna ya kwanza linatumia gharama kubwa sana kuboresha teknolojia ya mitambo na mashine zake na mara nyingi hufanya hivyo baada ya kupitwa na wakati kwa mbali sana, hivyo viwanda hivyo huendeshwa na soko badala ya kuliendesha soko, Taifa linapowekeza zaidi katika viwanda hivi bila kuwekeza katika utafiti wa teknolojia na viwanda mama ambavyo ndiyo huviwezesha viwanda hivyo kiteknolojia, basi viwanda hivyo haviwezi kuhimili ushindani katika soko huria ambalo limejaa bidhaa toka kila kona ya dunia
Lakini uwekezji katika namna ya Pili, yaani teknolojia mama, ni mgumu na wa gharama kubwa sana kwani unagusa fani nyingi tofauti tofauti na wakati mwingine ambazo hazina uhusiano wa moja kwa moja na bidhaa lengwa. Kwa jumla tunapozungumzia kuwekeza kwenye technolojia ya viwanda mama tunapaswa kufikiria mfumo mzima wa utafiti na uendelezaji teknolojia. Mfuno huu unahusisha miongoni mwa mambo mengi, yafuatayo; Ukusanyaji wa taarifa za kisayansi na teknolojia (Intellectual Property Resources and Technology Transfer), utunzaji wa taarifa hizo na namna ya kuzifikisha kwa walengwa ambao ndiyo watumiaji, Tafiti za kisayansi (Research & Development) na namna unavyowawezesha wataalam kufanya tafiti, kujaribu mawazo yao na kuunda vifaa vipya kwa ajili ya majaribio ya kisayansi, Ubunifu na usanifu (Design, Development and Innovation) wa bidhaa na mifumo mipya ya ualishaji na namna ya kuhakisha ubora na viwango
Tunapozungumzia uwekezaji katika teknolojia hatumaanishi wawekezaji wageni ambao wao dhamila yao kubwa ni kukusanya faida kubwa iwezekanavyo toka kwenye kile wanachowekeza na siyo kuinufaisha nchi, tumeona jinsi wawekezaji wanavyofanya kila linalowezekana kukwepa kulipa kodi za serikali pamoja na faida kubwa wanayoipata kutokana na rasilimali zetu. Uwekezaji unaofanywa na watu hawa ni ule tu unaowaongezea wao tija, nafasi ya kuaminika na kujiongezea faida zaidi.
Tunaposema tuwekeze katika teknolojia tunamaanisha; kusomesha wataalam wetu wenyewe, kuthamini kazi za wataalam ambao tayari tunao na kuwahakikishia mazingira mazuri ya kazi, kuwapatia wajasiliamali wetu mitaji bila kujali itarudi lini na kuwawezesha kiteknolojia. Swala hili ni gumu sawa kabisa na swala la kusomesha watoto kwa mzazi asiyejua maana ya elimu kwa wanawe. Mzazi huyu anaona mzigo kutoa sehemu ya mapato yake kusomesha watoto wake mwenyewe kwa kuwa tu, hata waliosoma au kusomesha wa kwao nao pia bado wanamaisha magumu. Lakini mzazi huyo huyo ndiyo wa kwanza kusifia mafanikio ya watoto wa jirani zake.
Watanzania ni lazima tuamue sasa kuwekeza kwenye teknolojia ama sivyo tuache kuota ndoto za maendeleo, vinginevyotutakuwa tunasubiri matokeo ya bahati nasibu yatangazwe kwa matumaini ya kushinda wakati hatukukata tikiti.
Moja ya matatizo makubwa yanayowakabili wajasiliamali wa Tanzania ni ubora duni na gharama kubwa sana za uzalishaj,i bidhaa za wajasiliamali wetu haziwezi kuhimili ushindaji hata katika soko la ndani tu. Katika hili kuna mambo makubwa mawili; Ubora na Gharama.
Tatizo la ubora linasababishwa zaidi na ufinyu wa mitaji na teknolojia hafifu zinazotumiwa na wajasiliamali wengi wa Tanzania, kukosekana kwa taarifa za kiteknolojia (Intellectual Property Resources), kukosekana kabisa kwa mifumo ya kufuatilia ubora na viwango vya malighafi na vifaa vya uzalishaji.
Vilevile uhaba wa wataalamu mbalimbali katika teknolojia kunapelekea ubora duni na gharama kubwa za uzalishaji katika viwanda vyetu vingi. Tanzania hatuna mfumo mzuri wa kuwatumia vizuri wataalamu wetu hasa wastaafu ambao ujuzi na uzoefu wao ungeweza kuwa nguzo muhimu sana katika ujenzi wa taifa letu. Hivi leo siyo ajabu kukutana na mtu uliyesoma naye darasa moja chuo kikuu wakati huo mkichukua degree ya uhandisi mitambo, akakuambia yeye ni mwanasheria au mhasibu wa taasisi fulani na hataki hata kusikia habari ya uhandisi. Haya yote ni matokeo ya kukosekana kwa uwekezaji wa uhakika kwenye teknolojia ya viwanda mama
Baada ya wajasiliamali kufanikiwa kutengeneza bidhaa zao, tatizo lingine ni namna ya kuziingiza sokoni, Tanzania hatuna mfumo madhubuti wa kuwaingiza sokoni wajasiliamali wazalendo zaidi ya maonyesho machache ya kibiashara yanayofanyika katika baadhi tu ya sehemu hapa nchini. Tumekuwa tukisikia mara nyingi viongozi wakisema “zalisheni bidhaa kulingana na mahitaji ya soko” bila ya kuainisha hayo mahitaji ya soko, lakini wakati huo huo wachina wanauza kila kitu katika soko hilohilo ambalo sisi tunashindwa kuuza, Mimi naamini kuwa katika teknolojia fursa huwa haziishi na kila kitu cha kiteknolojia kinaweza kuuzika bila kujali kimetoka wapi, cha msingi ni ubora na gharama, kisha kinachofuata ni mfumo wa kuuza ambao kwa bahati mbaya hatunao.
Kimsingi watanzania wote sasa tunawajibika kuchukua hatua kila mmoja kwa nafasi yake kwa kushirikisha serikali, na wadau wengine wa maendeleo kuweka mazingira mazuri kwa wataalam wetu na kuwaleta pamoja wanasayansi, wahandisi, wahitimu a vyuo vikuu, wajasiliamali na wadau wengine katika kutafuta majibu ya kiteknolojia kwa matatizo na changamoto zilizopo katika jamii zetu. Serikali kwa upande wake inapaswa kuweka vipaumbele kwa wawekezaji wanje kwenye maeneo yale tu ambayo yatatusaidia kuwapatia wataalam wetu ujuzi na utaalam hasa kwenye eneo la teknolojia ya hali juu sana (hi-tech). Ikibidi kuwe na utaratibu maalum wa kuwaelekeza wawekezaji maeneo mahsusi ambayo wataalam wetu watajifunza na kuambukizwa teknolojia ambayo nao wataitumia kwa manufaa ya taifa. Kwenye hili tutapata tabu sana hasa kwenye masuala ya haki miliki, lakini lazima tujue kwamba kwa sasa kila mtu anatamani kuwa rafiki yetu iwe wa kinafiki au wa kweli, hivyo huu ndiyo wakati wetu tunaopaswa kuchuma kutokana na lasilimali zetu vinginevyo tutaliwa! Asietaka kufungua haki miliki zake ili afaidike na rasilimali zetu tumwache aende wako wengi tu wengine watakuja, wala hatuna haja ya kufanya haraka, kwani rasilimali zetu aziozi wajukuu zetu watazikuta kama sisi tulivyozikuta. Ninaposema tuwekeze kwenye teknolojia sina maan kwamba tukianza kuwekeza leo, basi kesho tutaweza kuunda jeti, hapana. Maana yake ni kuwa tukianza kuwekeza sasa na kuweka mazingira bora kwa wataalam wetu kupata teknolojia hizo itakuwa ni mtaji mzuri sana hapo baadaye kuweza kuunda vifaa vya teknolojia ya hali ya juu sana kama vile ndege za jets.
Serikali inahitaji kueweka utaratibu mahsusi wa kusimamia tafiti za kisayansi, kugharamia uendelezaji wa teknolojia na kusomesha wataalamu kulingana na mahitaji ya wakati husika, Kuondoa pengo la kiteknolojia kati ya nchi yetu na mataifa yaliyoendelea, kwa kufanya uchunguzi wa kiintelijensia kujua ubunifu na hatua zinazofanywa na wanasayansi kwingineko duniani ili kuepuka mshangao (surprise) toka kwa washindani wetu. Kushiriki kikamilifu katika kufanya tafiti na kuendeleza teknolojia muhimu kwa mahitaji ya wananchi wa mijini na vijijini, kukuza uwezo wa wajasiliamali kuanzisha na kuendesha biashara za uzalishaji kiushindani na kwa ufanisi, kuhamasisha kuanzishwa kwa viwanda vingi vidogo vidogo ambavyo vitatumia teknolojia rahisi kuvuna rasilimali zetu kwa manufaa ya wote na sio watu wachache wenye uwezo,  pia kulinda na kutunza mazingira yetu
Tunahitaji kuwa na taasisi za kutosha ambazo zitakuwa kama macho yetu kwa ulimwengu wa nje wa sayansi na teknolojia, kwa lengo la kukusanya, kutunza na kusambaza taarifa za kisayansi na kiteknolojia kwa wadau pale zinapohitajika kwa wakati na ubora.
Tunahitaji vituo mbalimbali vya kusimamia na kuendesha tafiti mbali mbali za kisayansi (mbali ya vyuo vikuu), kufanya majaribio ya kisayansi na kubuni na kuzifanyia utafiti teknolojia mbali mbali na kuzitolea taarifa (Technical Reports)
Vituo vya Usanifu na Ubunifu - Design, Development & Innovation Administration; vituo hivi vinajukumu kuwasaidia wataalamu na wajasiliamali wetu la kutafsiri matokeo ya tafiti za sayansi na teknolojia kuwa katika vitu halisi, inawajibika kubuni bidhaa mbali mbali kutokana na matokeo ya tafiti na mahitaji soko, kuandaa michoro pamoja na kutengeneza prototype, na kufanya majaribio na mpangilio wa uzalishaji. Kubuni na ketengenza mfumo mzima wa uzanishaji wa vifaa husika ili kukidhi mahitaji.
Vituo vya uwekezaji na msaada wa kiufundi wa viwanda vidogovidogo SMEs Development & Support – kuwasaidia wajasiliamali wa Tanzania kuweza kuanzisha viwanda vidogo vidogo na kuhakikisha kuwa bidhaa wanazozitengeneza zinakidhi viwango vya ubora na vinaweza kuhimili ushindani wa soko huria

Wednesday, November 20, 2013

Tunahimiza mapinduzi ya teknolojia katikati ya nguvu za giza!


Bundi: Alama/Ishara ya ushirina na uchawi
Mabadiliko katika tasnia ya sayansi na teknolojia, uchumi wa kisasa na mfumo wa utandawazi na soko huria, umelata mabadiliko makubwa sana katika mfumo wa maisha ya watu wengi katika mataifa mengi duniani husasi nchi masikini za dunia ya tatu kama Tanzania ambazo uchumi wake unategemea sana uchumi wa  nje.
Mapinduzi ya kiteknolojia yanatokana na kazi za utafiti wa kiasayansi na siyo matunguli
Kwa ujumla kuna watu wengi ambao wameneemeka na mabadiliko hayo ya uchumi kwani yameletea fursa nyingi za kiuchumi  ambazo hapo mwanzo hawakuwa nazo kutokana na mfumo wa biashara uliokuwapo hasa wakati wa vita baridi iliyomazika mwishoni mwa miaka ya themanini.  Watu waliopokea mabadiiko hayo kwa mtazamo chanya zaidi wameweza kujilimbikizia fedha na mali nyingi katika kipindi kifupi sana ukilinganisha na wakati mwingine wowote ule ambao dunia imekuwa ikipitia katika misuko suko ya kiuchumi kama hii ya sasa. Biashara nyingi zimenzishwa, teknolojia mpya zinagunduliwa kila uchao na mamilioni ya watu wanafurahia na kufaidi matunda ya uhuru wa habari na mawasiliano, uhuru ambao hautambui mipaka ya kijiografia wala ya kiitikadi. Hivi sasa watu waliopo katika maeneo tofauti kijiografia wanaweza kuendesha na kufanya vikao, mikutano, makongamano, semina na hata majadiliano ya kibiashara bila ya kujali umbali baina yao utadhani wote wapo katika chumba kimoja. Heko teknolojia ya habari na mawasiano.
Wakati wanasayansi wenzetu wanaota kuishi nje ya sayari ya dunia,
 sisi tunamikakati gani ya kuelekea huko?
Katika nchi yetu matunda ya maendeleo yaliyotokana na mabadiliko ya hayo hayajaweza kuwafikia na kuwafaidisha watu wengi sana kama ambavyo ilitarajiwa. Zaidi ya kuwa mabadiliko hayo yamenaonekana kuwanufaisha zaidi watu wachache katika nchi yetu ambao wengi wao ni wafanyabiashara, wanasiasa katika ngazi za juu za utawala na maamuzi na wasomi wa daraja wa daraja la kati wanaojipatia kipato kikubwa kutokana na fursa walizonazo katika ajira zao. Masikini na watu wenye kipato cha kawaida wameachwa pembezoni wakiwa watazamaji bila ya matumaini wala matarajio yoyote. Jambo hili limepelea kuzidi kuongezeka kwa pengo kati ya walionacho na wasionacho kwa kiasi ambacho kama hatua za makusudi hazitachukuliwa basi muda si mwingi ujao huwenda inchi yetu ikawa si mahali salama sana per kuishi kama tulivyozowea.
Wakati wachawi wakitumia unga, fagio na pembe na vitu vingine visivyoonekana kusafiria, wanasayansi wana fanya kazi kubwa kugundua na kuunda mashuine halisi zinazoleta mapinduzi ya kweli kwa mmaisha ya watu
Wakati ambapo baadhi ya watu waliofanikiwa kwa kiasi kikubwa katika maisha wakionekana kama mfano wa kuigwa katika jamii yetu kuna jamba moja ambalo kwa kweli linatia hofu japo kwa sasa inaonekana kama sehemu muhimu sana katika maisha. Sio ajabu hapa nchini kusikia kuwa baadhi ya watu maarufu wakiwemo wanasiasa, wafanyabiashara na wafanyakazi bila kujali kiwango cha ufahamu au elimu zao kuwa mafanikio waliyonayo yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na nguvu za giza! Tumeshazowea kushuhudia wanasiasa wakipishana bila idadi kwa sangoma kule mlingotini wakisaka ubunge au madaraka mengine ya kisiasa! Inashangaza sana kwamba viongozi wetu hawaamini kama watu waliowachagua walifanya hivyo hivyo kwa kuwaamini matokeo yake wanatafuta mbinu za kichawi ili kuwaroga wapigakura wao au mabosi wa ili wawachague na kuwapa ulaji wanaoutaka. Tunajua viongozi wengi ambao wanapata madaraka kwa njia za kichawi, mara nyingi hawajiamini kwenye manbo ya kimsingi lakini majibu yao yamejaa kiburi, jeuri na kejeli, wanajua watu waliowapa madaraka walionayo hawana uwezo wa kuwaondoa kwani hata hivyo hawakuwapa kwa dhamira zao binafsi bali kwa nguvu za giza
Wafanyabiashara kwa upande wao nao kila kukicha wanashindana kwa waganga kutafuta madawa ya kuvuta utajiri zaidi na kung’arisha nyota zao, wao wapo tayari hata kutoa uhai wa binadamu wenzao ilimradi tu wapete mali zaidi, huu ni ubinafsi uliovuka mipaka kiasi ambacho huwezi kuelezea, wengine wamedirika hata kufanya ngono na wazazi wao ili wapate hiyo mali na utajiri wanaousaka usiku na mchana. Hali haiko tofauti huko maofisini, ambako wafanyakazia katika kada mbalimbali nao wanakesha kwa wataalam kutafuta bahati ya kupandinshwa cheo, kulinda kazi zao zisiwaponyoke, au kuongezwa mishahara na kupewa upendeleo katika mambo mbalimbali ya kikazi. Kwa maaskofu na mashehe huko hali ndiyo mbaya zaidi, sasa siyo ushirikina peke yake, wapo baadhi wanauza hata madawa ya kulevya kupitia makanisa yao!


Mganga wa kienyeji mitaani Afrika Kusini
Hali inatisha zaidi pale serikali inaposhadadia nguvu zisizoonekana kwa kisingizio cha kuiombea nchi, wanasiasa hawajiulizi mara mbili kuwakusanya wananchi kwa maelfu kufanya maombi pale taifa linapokabiliwa na tishio fulani iwe la kisiasa, kiuchumi au kijamii. Kwenye michezo hili ndiyo imekuwa ada, bila maombi timu zetu hakuna kitu, utamsikia kiongozi wa soka akiwahimiza wananchi “ndugu wananchi tuiombee timu yetu ya taifa katika mchezo wa leo iweze kushinda kwani mchezo huu ni wa muhimu sana…” utadhani wapinzani wetu wao hawamjui Mungu au tunategemea mwenyezi Mungu amtume roho mtakatifu kama alivyofanya kwa wale mitume 11 wa bwana Yesu ili waweze kucheza na kupata ushindi. Naomba hapa ieleweke kwamba sipingi kumuomba mwenyezi Mungu kwa lolote lile, tatizo langu liko kwetu sisi wenyewe, kuwa tumefanya nini kilichondani ya uwezo wetu kuweza kufanya vizuri kabla hatujamgeukia Mwenyezi Mungu? Au ndiyo tunategemea muujiza kama ule wa babu wa Loliondo?  Hii inatisha sana hasa kwa taifa changa kama letu ambalo tunahitaji kukimbia kisayansi na kiteknoljia wakati wenzetu wanatembea ili tuweza kuondoa pengo la kimaendeleo baina yetu na mataifa mengine.
Pengine hatuwezi kushangaa sana kuwa hata serikali inashabikia imani za giza, kwa kuwa baadhi ya hao viongozi wanaoongoza hiyo serikali yenyewe pia wanaamini kuwa madaraka yao yametokana na msaada wa kichawi au nguvu za giza. Tunategemea nini kipya toka kwa viongozi kama hao? Tutakuwa wehu kama tutafikiri kuwa watu wanaweza kubadilika na kusaliti miungu wao, kamwe hawawezi kukemea mambo hayo pamoja na ukweli kuwa wanaelewa vema madhara yake kwa taifa letu na vizazi vyake.
Wengi huamini kuwa wachawi wanauwezo wa kufanya mambo ya ajabu 
ambayo hayawezekani kisayansi ikiwemo kusafiri kwa kutumia fagio, ungo, pembe n.k 
bila kujali elimu wala kanuni zinazotawala mwenendo wa dunia
Lakini labda mtu anaweza kujiuliza kuwa “ni kwa nini tunapinga imani hizi za kishirikina wakati kuna watu wengi wameweza kupata mafanikio makubwa sana na kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa?”
Kwanza kabisa ni lazima tuelewe kuwa ushirikina ni ishara ya wazi ya mtu aliyeshiwa mbinu na mikakati ya kimaisha, ni alama ya mtu ambaye hana jipya katika fikra zake na amefika mahali haoni suluhu yoyote ya matatizo yanayomkabili iwe ya kiuchumi, kijamii, kisiasa au hata mahitaji ya binfsi ya kibinadamu. Mtu anapofikia hatua hiyo hukabliwa na msongo wa mawazo na ni rahisi sana kushawishika kuingia kufanya jambo lolote lile litakaloelekea kumpatia ahue ya muda bila kujali athari za baadaye za matendo yake.
Wataalamu wakifanyia majaribio "Memory" ya simu ya mkononi, 
ushirikina hauwezi kwenda sambamba na kazi za kisayansi!
Tatizo kubwa la imani hizi za kishirikina ni kuwa zinadhoofisha na kudumaza kabisa uwezo wa watu wa kufikiria (Brainstorming Power). Wanashindwa kuona nguvu na uwezo uliyomo ndani yao, wanaweka kando elimu zao na hawaamini tena vipaji vyao, matokeo yake wanakuwa watumwa wa matapeli wanaojiita wataalam  ambao wameena na mabango yao kila kona za miji yetu wakichuma bila jasho mali za wajinga (wajinga ndiyo waliwao). Matapeli hawa wamekuwa wajanja sana na wanatumia mbinu za hali ya juu utaalamu wa masoko na saikolojiainu zao kwa kufuata maitaji ya wakati husikana ni wepesi sana kusoma hisia za wateja wao na wanajua sana namna ya kushughulika na hisia zao.
Jambo moja kubwa ambalo tunaweza kujifunza kutokana na biashara hii ya nguvu za giza na ambalo linaweza kuwa na manufaa makubwa jamii yetu ni namna watu hawa wanavyoweza kucheza na akili wa watu na kufanya kila kitu kionekane kuwa halisia, hisia hizo huwafanya watu hao kuwa na imani kubwa kiasi ambacho hawaamini kabisa kwamba kuna kushindwa katika maisha wakiwa na nguvu za giza. Nguvu hizo huwa kubwa kiasi cha kumfanya muhusika kufanya jambo lolote katika maisha bila kujali kupata athari mbaya, watu hawa huvaa ushujaa ambao unawafanya wasiweze kushindwa kitu. Lakini kutokana na ukweli kuwa watu wetu hawana elimu ya jinsi akili na ubongo wa binadamu unavyofanya kazi wanadhani ni damu za mbuzi au viungo vya albino vinavyowaletea mafanikio, jambo ambalo yawezekana likawa na ukweli japo ni kweli pia kuwa waganga wengi ni matapeli na dawa zao hazina owezo huo.
Uchawi pia unahusishwa na nguvu na uwezo wa ajabu unaopita uhalisia wa kibinadamu
Zama hizi ambazo sayansi na teknolojia vinatawala kila kitu watanzania tuna kazi ya ziada kuwaelimisha wanachi wetu juu ya kanuni za zinazotawala mfumo wa fahamu wa mwanadamu na mawasiliano ya nafsi. Kanuni hizo ni muhimu sana kwa mafanikio ya mtu mmoja mmoja na jamii nzima kwa jumla. Hivi sasa msisitizo mkubwa kwa wanachi na wasomi katika jamii zetu ni kujiajiri katika sekta binafsi jambo ambalo kama hatuna maandalizi mazuri kwa watu wetu tutaishia kwa wachawi na matapeli. Tunapashwa kama taifa kuwaandaa watu wetu kisaikolojia na elimu inayotawala kanuni za mafanikio, matumizi sahihi ya fedha, uewekezaji, masoko n.k. elimu hii haitolewi katika vyuo wala mashule yetu na watu wanaotoka katika vyuo hivyo huwa hawajui chochote kabisa kitu kinachowaingiza kwenye matumizi ya anasa nayasiyokuwa na maana matokea yake wanishia kukimbilia kwa masangoma.
Watu ambao tumekuwa tukidhani kuwa ni wasomi na wataalamu wa mambo mbali mbali katika jamii na ambao tunawamini kutushauri kila siku kwenye biashara zetu n.k. utkakuta kuwa wao wenyewe hawana kitu na hata hizo biashara wanazoshauri wao hawazifanyi – utakutana na mtaalamu elekezi wa biashara anashauri juu uendeshaji wa maduka lakini yeye menyewe hata genge linamshinda kusimamia. Tunayaona haya kwenye mikataba mbalimbali ambayo wataalam wetu wanaiingizwa mkenge aidha kwa makusudi au kwa kutojua.  Wanahubiri yale wasioyatenda, ambavyo wao wenyewe hawayaamini lakini mwisho wa siku lawama zote wanatupiwa wananchi masikini kwa ujinga wao.
Safari ni ndefu lakini lazima tuianze sasa! Hatuna muda zaidi wa kusubiri vinginevyo tuwe tayari kujisalimisha kwa wakoloni kwa mara nyingine watutawale na kutupa mkate wa siku huku tukiwa makolokoloni na mayaya majumbani kwao na wao akifanyakazi kwenye miradi ya kuhamisha rasilimali za taifa letu.


Monday, November 18, 2013

Maendeleo ya teknolojia hayaji kama mvua, tujitoe tuwekeze!



Wakati taifa letu lina umri wa zaidi ya miaka 50 tangu tujitwalie uhuru toka kwa wakoloni mwaka 1961, nadhani ni wakati mwafaka kwetu watanzania kujiuliza  kama kwa muda wote huo ni nini tumefanya kwa ajili ya maendeleo ya taifa letu, je hapa tulipo ndipo tulipotarajia kuwepo? Kama jibu ni ndiyo je sasa tunaelekea wapi na tutafikaje! na kama jibu ni siyo, ni kwanini tupo hapa na tunafanya nini ili kurudi kwenye mstali wa matarajio yetu? Ili tuweze kuelewa vizuri mantiki ya kujiuliza haya ni vema tukaweka mbali ushabiki wa kisiasa na siasa zisizokuwa na tija kwa kuzungumzia watu badala ya mambo ya msingi yanayoligusa taifa letu. Nasema hili kwani ni kawaida yetu kuingiza siasa kila mahali hata ambapo haistahili kuwepo siasa, watu waliofilisika kifikra wakati wote wao wanafikiria kulinda au kujenga “status” zao tu na kwa gharama yoyote ile bila kujali maslahi mapana ya taifa letu, watu hawa ni hatari na hawafai kuendekezwa kwani kwao kila jambo ni siasa tu.

Uundaji wa wa ndege kubwa kuliko zote duniani kwa sasa Airbus 380 ni matokeo ya uwekezaji mkubwa uliofanywa kwa pamoja na kwa ushirikiano baina ya wanasayansi, serikali na wadau wengine
 Katika nchi yetu hivi sasa kumefurika bidhaa za kila aina kutoka kila kona ya dunia, miongoni mwa bidhaa hizo ni zina toka katika mataifa ya mashariki ya mbali yakiongozwa na ndugu zetu wachina, hivi sasa Tanzania tunaagiza toka nje karibu kila kitu kuanzia vijiti vya kuchokolea meno, pamba za kusafishia masikio hadi zana za kisasa za teknolojia ya hali ya juu kama eropleni za mizigo na abiria magari meli kompyuta, simu vifaa vya kitabibu nk. Nyingi ya bidhaa hizo hazina ubora maridhawa maarufu kama bidhaa za kichina, kwani hazidumu kwa muda mrefu kama ilivyozoeleka kwa bidhaa tooka nchi za kimagharibi yaani ulaya na marekani. Kwa jumla ni kwamba wachina kwa sasa ndiyo wanaotawala soko la bidhaa za kiteknolojia hapa nchini na ni ukweli usiopingika kwamba hivi sasa wachina wanagusa maisha ya kila raia wa Tanzania kwa bidhaa zao, na naweza kwenda mbali zaidi kuwa hata watoto ambao hawajazaliwa, tumboni mwa mama zao, maisha yao yanaguswa na uwepo wa bidhaa za wachina.
Hali hii ya wachina kutawala soko la teknolojia hapa nchini siyo bahati mbaya wala haikuja kama mvua tu, bali ilikusudiwa na kuwekewa mikakati ya makusudi kabisa na selikali ya uchina na kufanyiwa kazi kwa dhati kabisa. Moja ya mikakati mkubwa ya serikali ya uchina ilikuwa ni kuvutia uwekezaji wenye tija katika maeneo maalum ambayo waliyachagua na kuyapa kipaumbe, wakati huo huo walihakikisha kuwa wataalamu wao hasa wahandisi wabunifu wanapatiwa fursa za kuwawezesha kujifunza toka kwa wawekezaji wakigeni kwa kufanya nao tafiti mbalimbali pamoja na kuendesha miradi kwa ubia kati wageni na wenyeji. Serikali ya china ilihakiksha inawapatia rasilimali za kutosha wataalam wake kuweza kunyumbulisha teknolojia walizojifunza kwa manufaa ya taifa lao. Serikali ya china pia ilihakisha kuwa sera na sheria za nchi zinasaidia zaidi kuwalinda wanasayansi wao na kuwapa msaada wa kila namna ili waweze kushindana kibiashara. Matokeo yake kila mtu anayajua, dunia nzima hivi sasa zimeenea bidhaa za kichina, Leo hii chochote utakacho fikilia katika masuala ya teknolojia utakipata uchina. Sisi je? Tupo wapi?

Wanafunzi mafunzoni: Wanaunda boti kama sehemu ya mafunzo.

Bila shaka tutakubaliana kwamba walichokifanya wachina sio uchawi, bali ni matokeo ya nia, madhumuni, jitihada na maamuzi magumu na makini waliyoyafanya. Nasema maendeleo na mafanikio ya uchina ya leo ni matokeo ya nia, madhumuni, jitihada na maamuzi magumu na makini yaliofanywa na viongozi wao miaka ya hamsini na sitini lakini yaliyotiwa nguvu mpya mwaka 1978 kwa mikakati ambayo imezaa mafanikio haya tunayoshudia leo.
Watanzania tunaweza kuwa kama au hata zaidi ya wachina kimaendeleo tukiamua, tunaweza kujifunza toka kwao kama tukitaka, tunaweza kufanya maamuzi magumu na makini sasa kwa manufaa ya vizazi vijavyo tukipenda. Nasema tukitaka au tukipenda kwa kuwa hatulazimishwi kufanya hayo, yote ni hiari yetu, hakuna atakaye tuuliza kwa nini hatuja fanya wala atakayetulaumu kwa kufanya. Lakini tukiamua kufanya basi tuweke siasa pembeni na tufanye kazi, kwani hatima yetu na  ya taifa letu imo mikononi mwetu. Tunaweza kuibali kama tutaamua kufanya hivyo, vinginevyo tunaweza kuendelea kupiga siasa kwenye kila kitu tunachofanya na kucheza michezo michafu na kujipendekeza kwa kina Fulani tukidhani watatuona wa maana na tunajua sana,  tusipo fanya tutaendelea kulaumu sana wakoloni na wachina, tutaendelea kuabudu mlingotini na kugombana kwa dini na makabila yetu wakati mifano tunayo dhahili.
NDUGU ZANGU TUAMUE SASA KUBADILIKA, TUTAKE TUWE KAMA WACHINA, TUNAJUA TUNAWEZA, SABABU TUNAYO, NIA TUNAYO NA RASILIMALI ZOTE TUNAZO, TUSIPOZITUMIA SISI RASILIMALI ZETU WATAZITUMIA WENGINE NA HATUTAWAZUIA! TUTABAKI TUNALALAMA TU HADI LINI?